Kwa maombi ya kazi, Bofya hapa
Kocha Mkuu wa Simba, Roberto Oliveira 'Robertinho' amesema anahitaji nyota wapya baada ya kukutana na mabosi wa Simba katika kikao cha tathmini.
Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Simba, Ahmed Ally, alisema katika kikao hicho kilichohusisha wajumbe wa bodi waliokuwa mkoani Lindi, Robertinho aliweka wazi anahitaji beki, viungo wawili (mshambuliaji na kiungo mkabaji) pamoja na mshambuliaji ambaye ana ubora zaidi ya Jean Baleke.
Ahmed alisema tayari kocha huyo ameshafanya maboresho ndani ya kikosi cha Simba ambacho kimekuwa na mwendelezo mzuri na anataka kuitengeneza timu hiyo ili iwe tishio kwa ndani na nje ya nchi.
"Baada ya mchezo wa marudiano dhidi ya Wydad Casablanca, Kocha Robertinho alifanya kikao na viongozi wa bodi tukiwa hotelini Morocco, kikubwa ni kutoa tathmini ya timu kufuatia ushiriki wa Ligi ya Mabingwa Afrika, na katika kikao hicho ametoa mapendekezo ya usajili wa wachezaji wapya,” alisema Ahmed.
Meneja huyo alisema anaamini wachezaji walioko wana ubora na kinachohitajika ni maboresho ambayo kazi yake imeshaanza kufanyika.
“Kocha amesema anapata changamoto kwa sasa kwa sababu ya mshambuliaji mmoja (Jean Beleke), aliyekuwa naye, lakini pia anataka mbadala wa Chama (Clatous), lengo ni kutengeneza kikosi bora na tishio katika ukanda huu wa Afrika na zaidi kufika hatua ya nusu fainali hadi fainali katika michuano ya kimataifa,” Ahmed alisema.
Kuhusu matokeo dhidi ya Namungo FC Robertinho amesema matokeo hayo yamewapunguzia presha wapinzani wao wakubwa, Yanga ambao wako katika mbio za kuwania ubingwa.
"Wachezaji walijitahidi kupambana, makosa madogo yalitugharimu lakini sasa tunaangalia mbele kwenye michezo ya ligi iliyobakia na Kombe la FA," alisema Robertinho.
Aliongeza alilazimika kupumzisha baadhi ya nyota wake wa kikosi cha kwanza kutokana na kukabiliwa na mchezo muhimu wa hatua ya nusu fainali ya FA dhidi ya Azam itakayochezwa Jumapili.
0 Comments