Ticker

6/recent/ticker-posts

Yanga Yambakisha Dickson Job, Apewa Mkataba Mnono

Kwa maombi ya kazi, Bofya hapa

Yanga imefanikiwa kumbakisha beki wake tegemeo Dickson Job katika kikosi cha timu hiyo chini ya Kocha Mtunisia, Nasreddine Nabi baada ya kumpa mkataba mnono.

Hiyo ikiwa ni siku chache tangu taarifa zienee za beki huyo kuwepo katika mazungumzo na Klabu ya Al Ittihad ya nchini Misri.

Ittihad hivi sasa inanolewa na aliyekuwa Kocha Mkuu wa Simba, Mserbia, Zoran Maki, aliyeusitisha mkataba wake wa miaka miwili mwanzoni mwa msimu huu kabla ya kutimka, Septemba 2022.

Kwa mujibu wa taarifa ambazo imezipata Spoti Xtra, kutoka ndani ya Kamati ya Mashindano na Usajili ya Yanga, pande mbili za uongozi wa timu hiyo, na menejimenti ya beki huyo zimefikia muafaka mzuri na kumpa mkataba wa mwaka mmoja.

Mtoa taarifa huyo alisema kuwa makubaliano hayo yamefikia pazuri, baada ya kuboreshewa baadhi ya mahitaji yake yaliyokuwepo katika mkataba wake huo mpya aliopewa.

Aliongeza kuwa, maboresho hayo yamefanyika katika sehemu ya mshahara wake ukiwa mkubwa zaidi ya ule wa awali aliokuwa anaupata.

“Yanga na menejimenti ya Dickson Job ambayo inamsimamia, kwa pamoja zimefikia muafaka mzuri na kukubaliana kuingia makubaliano ya kusaini mkataba wa mwaka mmoja.

“Makubaliano hayo ni mazuri yenye maslahi makubwa kwa mchezaji baada ya kuomba kuboreshewa baadhi ya mahitaji yake katika mkataba huo mpya.

“Kati ya maboresho hayo ni mshahara atakaoupata katika kila mwezi kwa kipindi ambacho atakuwepo Yanga, na hiyo ni baada ya kupata taarifa za kuhitajika na baadhi ya klabu za nje ya nchi,” alisema mtoa taarifa huyo.

Rais wa Yanga, Injinia Hersi Said, alizungumzia hilo la usajili na kusema kuwa: “Hatutakubali kumuachia mchezaji yeyote mkubwa kuondoka katika timu yetu.

“Kama yalivyokuwa malengo yetu hivi sasa ni kuhakikisha tunatengeneza timu bora na imara katika Ukanda wa Afrika, hivyo kila mchezaji muhimu na tegemeo hataondoka Yanga,” alisema Hersi.

Post a Comment

0 Comments