Manzoki alisema ni kweli ana mkataba na Vipers lakini hauzidi miezi mitatu na hizo taarifa kwamba ni wa miaka miwili ni udanganyifu ambao tayari menejimenti yake imeanza kulishughulikia na asingependa kulizungumza kwa undani zaidi.
Akizungumza katika mahojiano maalumu, Manzoki alisema klabu ya Vipers inajua mkataba baina yao umebaki wa muda gani na kama wataendelea kushikilia hilo la miaka miwili kuwa eti atamaliza kuitumikia Vipers 2025, hatakwenda mazoezini, katika mechi wala shughuli yoyote ya timu hiyo.
“Muda niliokwambia umebaki kwenye mkataba wangu ndio sahihi, hilo jingine wala silifahamu na naamini baada ya kufikia ukingoni nitaondoka hapa Vipers kwenda katika timu nyingine,” alisema Manzoki na kuongeza;
“Nitakuja kucheza hapa Tanzania na klabu yangu mpya itakuwa Simba, hilo si suala la kuficha tena kutokana na kitu ambacho wamekifanya Vipers wala sijapendezewa nacho na si vizuri.”
Manzoki aliyeiwezesha Vipers kubeba ubingwa wa Uganda msimu uliopita, alifafanua; “Wakala wangu yupo katika mazungumzo mazuri na viongozi wa Simba na kilichokuwa kimekwamisha ni hiyo miezi michache iliyobaki katika mkataba wangu na si kama wao walivyoeleza si jambo la kweli.
0 Comments